Timu ya Taifa ya Misri imeandika historia kwa kutinga hatua ya 32 Bora ya Kombe la Dunia 2026 baada ya kutoka sare ya mabao 1-1 dhidi ya Iran katika mchezo wa mwisho wa Kundi G uliochezwa Seattle.
Matokeo hayo yaliifanya Misri kumaliza hatua ya makundi ikiwa na alama tano baada ya kucheza mechi tatu bila kupoteza, huku Belgium ikiibuka kinara wa kundi hilo kwa tofauti ya mabao kufuatia ushindi mnono wa mabao 5-1 dhidi ya New Zealand katika mchezo mwingine wa kundi hilo. Iran, iliyomaliza nafasi ya tatu, imelazimika kusubiri hatima yake kupitia orodha ya timu bora zilizomaliza nafasi ya tatu.
Misri ndiyo ilikuwa ya kwanza kupata bao kupitia Mahmoud Saber, aliyeitumia vyema makosa ya kipa wa Iran, Alireza Beiranvand, na kuiweka timu yake mbele. Hata hivyo, Iran ilisawazisha kupitia Ramin Rezaeian, baada ya shambulizi lililofuatia kipa wa Misri kuokoa mkwaju wa penalti uliopigwa na Mehdi Taremi.
Dakika za mwisho zilikuwa za kusisimua baada ya Iran kufunga bao ambalo lingeweza kuwapa ushindi kupitia Shoja Khalilzadeh, lakini baada ya mapitio ya VAR, bao hilo lilikataliwa kwa madai ya kuotea, na mchezo ukamalizika kwa sare ya 1-1 iliyotosha kuipa Misri tiketi ya hatua ya mtoano.
Wakati huo huo, Belgium ilionyesha ubora wake kwa kuichapa New Zealand mabao 5-1 na kujihakikishia nafasi ya kwanza katika Kundi G. Leandro Trossard alikuwa nyota wa mchezo huo baada ya kufunga mabao mawili, huku Kevin De Bruyne, Romelu Lukaku na Alexis Saelemaekers wakiongeza bao moja kila mmoja. Bao la kufutia machozi la New Zealand lilifungwa na Elijah Just katika kipindi cha pili.
Katika hatua ya makundi, Misri ilianza kwa sare ya 1-1 dhidi ya Belgium kabla ya kuibuka na ushindi wake wa kwanza kabisa katika historia ya Kombe la Dunia kwa kuifunga New Zealand mabao 3-1. Ushindi huo uliambatana na mabao ya Mostafa Zico, Mohamed Salah na Mahmoud Trezeguet, kabla ya kumaliza kampeni ya makundi kwa sare dhidi ya Iran.
Kwa kufuzu huko, Misri na Belgium sasa wanasubiri kujua wapinzani wao katika hatua ya 32 Bora, huku matumaini ya Wafarao yakibaki makubwa chini ya nahodha wao Mohamed Salah, ambaye ameiongoza timu hiyo kufikia hatua ya mtoano kwa mara ya kwanza katika mfumo mpya wa Kombe la Dunia wenye timu 48.



