Mechi za ligi kuu ya NBC raundi ya 29 zimehitimishwa leo kwa vigogo wa soka nchini Ynga na Simba kuendelea kuchuana kwenye mbio za ubingwa baada zote kushinda.
Ikicheza uwanja wa KMC Complex, Yanga ikiwaadhibu TRA United mabao 3-0 kiungo mshambuliaji Allan Okello akifunga hat-trik ya nne msimu huu.
Ushindi huo umeifanya Yanga ifikishe alama 72 na kuendelea kusalia kileleni mwa msimamo wa ligi kwa tofauti ya alama mbili dhidi ya wapinzani wao Simba.
Simba ilikuwa uwanja wa Isamuhyo ikichuana na Singida BS katika mchezo ambao Wekundu wa Msimbazi waliendeleza ubabe kwa ushindi wa mabao 2-0.

Elie Mpanzu na Anicet Oura walifunga mabao hayo na kuwahakikishia Wekundu wa Msimbazi alama tatu muhimu zilizowafanya wafikishe alama 70.
Azam Fc nayo ilikuwa mkoani Tanga kuikabili Coastal Union wakiibuka na ushindi wa mabao 2-0 katika mchezo uliopigwa uwanja wa Mkwakwani.
Feisal Salum alifunga bao lake la 15 katika mchezo huo na kuendelea kuongoza mbio za ufungaji bora mbele ya Okello na Mossi Ndumumwe wenye mabao 14 kila mmoja.
Chini ya msimamo kuna mabadiliko yametokea baada ya Tanzania Prisons kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Mtibwa Sugar na kuondoka eneo la hatari kushuka daraja moja kwa moja wakiishusha Mtibwa Sugar ambayo sasa inachungulia kaburi.






