Hatua ya makundi ya Kombe la Dunia 2026 imehitimishwa rasmi, huku timu 32 zikifuzu kwenda hatua ya mtoano itakayoanza leo. Baada ya wiki kadhaa za ushindani mkali, mataifa yaliyoshindwa kufanya vizuri yameaga mashindano, na sasa kila mchezo utakuwa wa kuamua hatma ya timu, ambapo mshindi atasonga mbele na aliyeshindwa ataondolewa.
Toleo la mwaka 2026 limeweka historia kwa kuwa la kwanza kushirikisha timu 48 katika hatua ya makundi. Mfumo huo mpya umeongeza ushindani mkubwa, huku mataifa kadhaa yakifanikiwa kuandika historia kwa kufuzu hatua ya 32 bora kwa mara ya kwanza, yakiwemo Cape Verde, Ivory Coast na Afrika Kusini, huku mataifa makubwa yakithibitisha ubora wao kwa kutinga hatua inayofuata.
Hatua ya makundi pia imeshuhudia matokeo ya kushangaza, baadhi ya vigogo wakipata wakati mgumu kabla ya kufuzu, huku mataifa mengine yakishindwa kutimiza matarajio na kuaga mapema mashindano. Ushindani mkubwa katika makundi umeonyesha kuwa tofauti ya viwango kati ya timu imeendelea kupungua, jambo lililofanya karibu kila mchezo kuwa na umuhimu mkubwa.
Kwa bara la Afrika, Kombe la Dunia hili limekuwa la kihistoria baada ya mataifa tisa kufuzu hatua ya 32 bora, idadi kubwa zaidi kuwahi kufikiwa na bara hilo katika historia ya mashindano hayo . Morocco, Afrika Kusini, Algeria, DR Congo, Ivory Coast, Senegal, Egypt, Ghana, Cape Verde sasa wanabeba matumaini ya Afrika katika hatua ya mtoano huku wakisaka nafasi ya kuendelea kuandika historia.
Hatua ya 32 bora inaanza leokwa mchezo baina ya Afrika kusini dhidi ya Canada na kufuatiwa na michezo kadhaa mikubwa inayotarajiwa kuvuta hisia za mashabiki duniani. Miongoni mwa mechi zinazosubiriwa kwa hamu ni Ujerumani dhidi ya Paraguay, Ufaransa dhidi ya Sweden, Uholanzi dhidi ya Morocco, Ureno dhidi ya Croatia, huku mataifa yote yakisaka tiketi ya robo ya mwisho ya mashindano.
Kuanzia leo, makosa hayatasamehewa tena. Kila dakika, kila bao na kila uamuzi unaweza kuamua hatima ya taifa. Baada ya hatua ya makundi kuhitimishwa na baadhi ya timu kuaga mashindano, sasa macho ya dunia yanaelekezwa kwenye hatua ya 32 bora, ambapo vita ya kusaka taji la Kombe la Dunia 2026 inaanza rasmi.



