Beki wa timu ya taifa ya Afrika Kusini, Mbekezeli Mbokazi, ameibuka kuwa mmoja wa nyota waliovutia zaidi katika Kombe la Dunia la FIFA 2026 baada ya kuonyesha kiwango cha juu katika mechi zote alizoichezea Bafana Bafana. Mbokazi, mwenye umri wa miaka 20, amevutia mashabiki, wachambuzi na vilabu mbalimbali kutokana na uwezo wake wa kujilinda na utulivu aliouonyesha katika mashindano hayo.
Mbokazi alizaliwa katika mji mdogo wa Hluhluwe, uliopo jimbo la KwaZulu-Natal nchini Afrika Kusini. Safari yake ya soka imekuwa ya kuvutia, ikianzia kwenye mazingira ya kawaida hadi kufikia kucheza kwenye jukwaa kubwa zaidi la soka duniani. Mwanzoni mwa mwaka 2026 alijiunga na klabu ya Chicago Fire FC ya Marekani akitokea Orlando Pirates kupitia mpango wa U22 Initiative wa Major League Soccer (MLS), unaolenga kuendeleza vipaji vya wachezaji vijana kutoka mataifa mbalimbali.
Ndani ya kipindi kisichozidi miezi sita tangu kuwasili kwake nchini Marekani, Mbokazi alijizolea nafasi katika kikosi cha MLS All-Star 2026 kabla ya kuitwa kujiunga na timu ya taifa ya Afrika Kusini kwa ajili ya Kombe la Dunia. Akizungumzia hatua hiyo, Mbokazi alisema mafanikio hayo yalikuwa kama ndoto iliyotimia na kwamba bado ana wakati mgumu kuamini alichokifikia. Alisema kila anapofikiria alikotoka na mahali alipo sasa, hujihisi mwenye fahari kubwa kuiwakilisha Afrika Kusini kwenye mashindano makubwa zaidi ya soka duniani.
Katika Kombe la Dunia, Mbokazi alianza kwa kucheza dakika zote 90 katika mechi ya ufunguzi dhidi ya Mexico, ambako licha ya Afrika Kusini kupoteza kwa mabao 2-0 na kumaliza mchezo ikiwa imepungukiwa na wachezaji wawili kutokana na kadi nyekundu, alisifiwa kwa kiwango chake cha juu cha ulinzi. Aliendelea kuonyesha ubora wake katika sare dhidi ya Czechia, ambapo mchango wake ulisaidia timu kupata penalti ya dakika za mwisho na kuondoka na pointi muhimu. Katika mchezo wa mwisho wa makundi dhidi ya Korea Kusini, Mbokazi alikuwa sehemu muhimu ya safu ya ulinzi iliyoiwezesha Bafana Bafana kushinda bao 1-0 na kufuzu hatua ya mtoano kwa mara ya kwanza katika historia ya timu hiyo.
Safari ya Afrika Kusini ilimalizika katika hatua ya 32 bora baada ya kufungwa bao 1-0 na Canada, lakini Mbokazi aliendelea kuthibitisha ubora wake kwa kuonyesha takwimu zilizomweka miongoni mwa mabeki waliofanya vizuri zaidi katika mashindano hayo. Alikamilisha mchezo akiwa na asilimia 91 ya usahihi wa pasi, alishinda dueli sita za ardhini, alifanya uokoaji mara tatu, aliingilia mipira mara mbili na kuzuia nafasi moja muhimu ya kufunga iliyoiweka timu yake kwenye ushindani kwa muda mrefu. Baada ya mchezo huo, kocha wa Afrika Kusini, Hugo Broos, alimpongeza Mbokazi kwa maendeleo yake makubwa, akisema ni mchezaji mwenye uwezo mkubwa ambaye bado ana nafasi ya kuendelea kukua na kuwa mmoja wa viongozi wa baadaye wa Bafana Bafana. Maonyesho hayo yameifanya thamani yake kuongezeka kwa kasi huku taarifa zikieleza kuwa vilabu kadhaa vya Ulaya vinafuatilia kwa karibu maendeleo ya beki huyo kijana. Kutoka kijana aliyelelewa Hluhluwe hadi kuwa mmoja wa nyota wa Kombe la Dunia 2026, Mbokazi ameandika sura mpya katika historia ya soka la Afrika Kusini na kuwa mfano wa jinsi vipaji vinavyoweza kufika kileleni vinapopata nafasi na maandalizi sahihi



