Dakika 90 za mwisho za NBC Premier League zimebeba vita nyingine nje ya uwanja, vita ya benchi la ufundi kati ya Kocha Mkuu wa Yanga, Abdi Hamid Moallin, na Kocha Mkuu wa Simba, Steve Barker.
Wote wawili wameonyesha uwezo mkubwa wa kuongoza timu zao msimu huu, lakini kila mmoja ametumia falsafa tofauti kuifikisha timu yake kwenye mbio za ubingwa hadi mchezo wa mwisho.
Moallin ameonekana kujenga Yanga inayocheza soka la kumiliki mpira, kushambulia kwa kasi na kutumia vizuri ubora wa wachezaji wake wa mbele. Chini yake, Yanga imekuwa ikipeleka presha kubwa kwa wapinzani kupitia pasi nyingi na uwezo wa kutengeneza nafasi za kufunga.
Pia ameonyesha uwezo wa kubadilisha mfumo kulingana na aina ya mpinzani anayekutana naye, jambo lililoifanya Yanga kubaki kwenye mbio za ubingwa kwa muda mrefu.
Kwa upande mwingine, Steve Barker ameijenga Simba kuwa timu yenye nidhamu kubwa ya kiuchezaji, uimara wa safu ya ulinzi na matumizi makubwa ya mashambulizi ya kushtukiza. Kocha huyo raia wa Afrika Kusini ameonyesha uwezo wa kusoma mchezo na kufanya mabadiliko yanayobadili matokeo, huku akiwapa wachezaji wake uhuru wa kutumia ubunifu katika maeneo ya mwisho ya uwanja. Sasa hesabu zote zimebaki kwenye dakika 90 za mwisho.
Yanga itaikabili JKT Tanzania ikiwa na nafasi ya kujimalizia kazi yenyewe, wakati Simba itakuwa na kibarua cha kuifunga KMC huku ikisubiri matokeo kutoka kwa wapinzani wao. Mwisho wa siku, ni mbinu, utulivu na maamuzi ya makocha hawa wawili yatakayoamua nani ataondoka akiwa bingwa wa NBC Premier League msimu huu.



