Kocha wa Young Africans SC, Abdihamid Moalin, ameweka wazi msimamo wa kikosi chake kuelekea mchezo wa NBC Premier League dhidi ya JKT Tanzania, akisisitiza kuwa Yanga haiingii uwanjani kwa lengo lingine lolote zaidi ya ushindi.
Akizungumza na waandishi wa habari leo, Moalin alisema maandalizi ya kikosi chake yamekamilika na wachezaji wako tayari kwa pambano hilo muhimu.
"Tunaingia kila mchezo kwa lengo la kushinda,"alisema Moalin kwa kujiamini, akionyesha dhamira ya mabingwa hao watetezi kuendelea na kasi yao bila kujali ukubwa wa mpinzani.
Kwa upande wake, kiungo Emmanuel Mwanengo alisema kikosi cha Yanga kinaelewa uzito wa mchezo huo, akibainisha kuwa ushindi wa aina yoyote utatosha kuipa timu hiyo ubingwa wa Ligi Kuu mbele ya mashabiki wao.
"Tunafahamu umuhimu wa mchezo huu na tumejiandaa vizuri. Lengo letu ni kushinda na kutwaa ubingwa,"alisema Mwanengo.
Kauli hizo zinakuja huku JKT Tanzania ikiwa tayari imeanza vita ya kisaikolojia kupitia mitandao ya kijamii kwa kuchapisha ujumbe wa "Last Dance", ikiashiria dhamira yao ya kuzuia Yanga kutwaa taji.
Hata hivyo, Yanga wamechagua kujibu kwa utulivu na kuonyesha imani yao kupitia maandalizi na kauli za viongozi wa kikosi, badala ya kuingia kwenye vita ya maneno.
Sasa macho yote yataelekezwa Uwanja wa Maj Gen Isamuhyo kesho saa 10:00 jioni, ambapo JKT Tanzania watakuwa wakisaka kuharibu sherehe za ubingwa, huku Yanga wakihitaji ushindi mmoja pekee kuandika historia nyingine. Dakika 90 za mchezo huo ndizo zitakazotoa jibu la mwisho.



