Uongozi wa Yanga SC umekanusha taarifa zinazosambaa kwenye mitandao ya kijamii zikidai kuwa klabu hiyo ipo katika mazungumzo ya kumuajiri kocha Fadlu Davids, ukisisitiza kuwa hakuna mazungumzo yoyote yaliyofanyika kuhusu suala hilo.
Kupitia afisa habari wa klabu hiyo Ally Kamwe, ameeleza kuwa taarifa hizo si za kweli na hazitokani na uongozi wa klabu. Uongozi huo umebainisha kuwa ongezeko la uvumi huo linachangiwa na hamu ya kutaka kupata taarifa za haraka kuhusu mipango ya klabu hiyo yenye maskani yake mitaa ya twiga na jangwani , hali inayowapa nafasi baadhi ya watu kusambaza taarifa zisizo na uthibitisho.
Klabu hiyo imewataka wanachama na mashabiki wake kuendelea kupata taarifa kupitia vyanzo rasmi pekee, ikieleza kuwa taarifa zote zinazohusu usajili wa wachezaji, mabadiliko ya benchi la ufundi na masuala mengine ya klabu zitatolewa kupitia YANGA APP pamoja na kurasa rasmi za Yanga SC kwenye mitandao ya kijamii.
Aidha, uongozi wa Yanga umefafanua kuwa taarifa yoyote kuhusu usajili wa kocha au mchezaji inayotolewa nje ya vyanzo hivyo rasmi inapaswa kupuuzwa hadi pale klabu itakapotoa tamko rasmi.
Wakati huo huo, Yanga imewataka mashabiki wake kuelekeza nguvu na umoja wao katika mchezo ujao wa NBC Premier League, ikiwahimiza kujitokeza kwa wingi uwanjani kuisapoti timu katika harakati za kutwaa ubingwa wa ligi msimu huu.



