Mabingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Yanga SC, wanakabiliwa na uamuzi mgumu kuhusu hatma ya mshambuliaji wao tegemeo, Prince Dube, baada ya mkataba wake kumalizika huku akitajwa kuwa kwenye rada za klabu kadhaa ndani na nje ya Afrika.
Taarifa kutoka vyanzo vya ndani ya uongozi wa Yanga zinaeleza kuwa nyota huyo wa Zimbabwe amewaomba viongozi wa klabu hiyo wamruhusu kutafuta changamoto mpya nje ya Tanzania, akiamini ni wakati sahihi wa kupiga hatua nyingine katika maisha yake ya soka baada ya kuitumikia Yanga kwa mafanikio makubwa kwa misimu miwili.
Chanzo hicho kimebainisha kuwa Dube tayari amepokea ofa kutoka klabu ya Kaizer Chiefs ya Afrika Kusini, huku pia akihusishwa na klabu za nchini kwao Zimbabwe ambazo ni Hardrock FC na Scottland FC.Β
Licha ya msimamo wa Dube kutaka kujaribu soka la nje, Yanga bado haijakata tamaa. Viongozi wa mabingwa hao wanaendelea na jitihada za kumshawishi nyota huyo kuongeza mkataba na kubaki Jangwani, wakiamini bado ana nafasi kubwa katika mipango ya benchi la ufundi kuelekea msimu mpya.
Awali kulikuwa na taarifa kwamba Yanga na Dube walikuwa kwenye mazungumzo ya kuongeza mkataba wake, huku pande zote zikionekana kukaribia makubaliano. Hata hivyo, taarifa za sasa kutoka ndani ya klabu zinaonyesha kuwa mshambuliaji huyo ameonyesha nia ya kutafuta changamoto mpya nje ya Tanzania.
Katika msimu uliomalizika, Dube alifunga mabao 10 na kubaki kuwa mmoja wa wachezaji muhimu wa Yanga. Mbali na uwezo wake wa kucheza kama mshambuliaji wa kati, pia ameonyesha ubora akiwa anacheza kutokea pembeni, jambo lililomfanya kuwa silaha muhimu katika safu ya ushambuliaji.
Katika mechi za mwisho za msimu dhidi ya Azam FC na JKT Tanzania, Dube alicheza zaidi akitokea pembeni, ambapo alitoa mchango mkubwa kwa kufunga na kutengeneza mabao
Pia amekuwa na kiwango kizuri akiwa na timu ya taifa ya Zimbabwe, hali iliyochangia kuongezeka kwa idadi ya klabu zinazomfuatilia kuelekea dirisha hili la usajili.



