Mabingwa watetezi Argentina wamefuzu hatua ya 16 bora ya Kombe la Dunia 2026 baada ya kuibuka na ushindi mgumu wa mabao 3-2 dhidi ya Cape Verde katika mchezo wa hatua ya 32 bora uliochezwa usiku wa kuamkia Julai 4.
Licha ya kutabiriwa kushinda kwa urahisi, Argentina ililazimika kupambana hadi dakika za mwisho za muda wa nyongeza dhidi ya Cape Verde, timu iliyokuwa ikicheza Kombe la Dunia kwa mara ya kwanza lakini iliyoonyesha kiwango cha juu kilichowavutia wengi duniani.
Nahodha Lionel Messi aliifungia Argentina bao la kwanza na kuendeleza rekodi yake ya mabao kwenye Kombe la Dunia, akifikisha mabao 20 katika historia ya mashindano hayo. Cape Verde ilisawazisha kupitia Deroy Duarte kabla ya mchezo kumalizika kwa sare ya 1-1 ndani ya dakika 90.
Katika muda wa nyongeza, Lisandro MartΓnez aliirejesha tena Argentina mbele kwa bao la pili, lakini Cape Verde haikukata tamaa na Sidny Lopes Cabral akaisawazishia timu yake kwa mara nyingine kwa bao maridadi lililoamsha matumaini ya kufika hatua ya mikwaju ya penalti.
Hata hivyo, dakika ya 111, shinikizo kubwa la Argentina lilizaa matunda baada ya mpira wa kichwa wa Cristian Romero kugonga beki Diney Borges na kujaa wavuni, bao lililohesabiwa kuwa la kujifunga na kuipa Argentina ushindi wa mabao 3-2.
Baada ya mchezo, kocha wa Argentina Lionel Scaloni aliisifu Cape Verde kwa ushindani mkubwa waliouonyesha akisema hakuna tena timu ndogo katika soka la kisasa. Naye Messi alikiri kuwa walijua tangu mwanzo kwamba wangekutana na upinzani mkali kutoka kwa wapinzani wao. Ushindi huo unaifanya Argentina kusonga mbele na sasa itakutana na Misri katika hatua ya 16 bora.
Cape Verde yaondoka kishujaa
Ingawa imeondolewa, Cape Verde imeandika historia kubwa katika ushiriki wake wa kwanza kabisa wa Kombe la Dunia. Taifa hilo dogo la visiwa lenye wakazi wasiopungua laki sita lilivutia dunia kwa soka lake la ujasiri, likiwabana mabingwa watetezi hadi dakika za mwisho za muda wa nyongeza.
Kipa mkongwe Vozinha alikuwa miongoni mwa nyota wa mchezo baada ya kuokoa mashuti mengi, yakiwemo kadhaa ya Messi, huku wachezaji wa Cape Verde wakiondoka uwanjani wakishangiliwa na mashabiki kutokana na kiwango walichoonyesha.
Afrika yabaki na wawakilishi wawili pekee
Baada ya matokeo ya hatua ya 32 bora kukamilika, bara la Afrika limebakiwa na timu mbili pekee katika hatua ya 16 bora:
Morocco
Egypt
Morocco ilitinga hatua hiyo baada ya kuiondoa Uholanzi kwa mikwaju ya penalti, huku Misri ikiandika historia kwa kushinda mchezo wake wa kwanza kabisa wa hatua ya mtoano wa Kombe la Dunia baada ya kuitoa Australia kwa penalti.
Timu nyingine za Afrika zilizoshiriki hatua ya mtoano Cape Verde, Ghana, Senegal, Algeria, Ivory Coast na DR Congo β zote zimeaga mashindano.
Kwa ushindi huo, Argentina itaingia hatua ya 16 bora ikiwa na kazi ngumu zaidi dhidi ya Misri, wakati macho ya wengi yakibaki kwa Lionel Messi ambaye anaendelea kuonyesha ubora wake kwa kuongeza idadi ya mabao yake katika historia ya Kombe la Dunia.



