Uongozi wa Yanga SC umeendelea na mchakato wa kusaka kocha mkuu mpya atakayechukua nafasi iliyoachwa na Pedro Gonçalves, lakini mipango ya awali ya kumleta kocha Fadlu Davids imekumbwa na changamoto na hatimaye mazungumzo kuvunjika.
Awali, mabingwa hao wa Tanzania Bara walikuwa kwenye mazungumzo ya karibu na Fadlu Davids, ambaye aliwahi kuzinoa klabu za Raja Casablanca ya Morocco na Simba ya Tanzania, kwa lengo la kumkabidhi jukumu la kuongoza kikosi hicho kuelekea msimu ujao wa mashindano ya ndani na kimataifa.
Sababu za kuvunjika mazungumzo
Kwa mujibu wa mwandishi na mchambuzi wa soka kutoka Afrika Kusini, Ayabonga Mthembu, pande zote mbili zimeshindwa kufikia makubaliano kutokana na tofauti kwenye masuala ya kifedha, hususan mfumo wa malipo na bonasi za mafanikio.
Taarifa hizo zinaeleza kuwa mazungumzo yalikuwa yamefikia hatua nzuri kabla ya kukwama katika vipengele vya mwisho vya mkataba, hali iliyosababisha Yanga kuhitimisha mazungumzo hayo kwa muda huo.
Baada ya dili hilo kugonga mwamba, Yanga sasa inaendelea na mchakato wa kumtafuta kocha mpya ambaye atakamilisha mradi uliowekwa na uongozi wa klabu hiyo.
Inaripotiwa kuwa huenda jina la kocha huyo mpya likafahamika ndani ya siku chache zijazo, pengine kabla ya mwisho wa wiki hii, huku uongozi ukiendelea kufanya tathmini ya wagombea waliobaki kwenye orodha fupi.
Hatma ya benchi la muda bado haijajulikana
Aidha, Yanga bado haijatoa tamko rasmi kuhusu hatma ya benchi la ufundi la muda lililoongozwa na makocha Abdihamid Moallin na Patrick Mabedi.
Makocha hao waliiongoza Yanga katika michezo saba ya mwisho wa msimu, ambapo walipoteza mechi mbili moja dhidi ya Dodoma Jiji kwenye Ligi Kuu na nyingine dhidi ya Azam FC katika nusu fainali ya Kombe la CRDB.
Hata hivyo, licha ya matokeo hayo, waliweza kufanikisha lengo kuu la msimu kwa kuisaidia Yanga kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu kwa mara ya tano mfululizo.



