Soka la Tanzania linatarajiwa kuingia katika enzi mpya ya matumizi ya teknolojia baada ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kutangaza mpango wa kuanza kutumia mfumo wa Video Support (VS) katika mechi za Ligi Kuu Tanzania Bara kuanzia msimu wa 2026/27.
Mfumo huo, ambao umeidhinishwa na Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA), unakusudiwa kusaidia waamuzi kufanya maamuzi sahihi katika matukio yenye utata kwa gharama nafuu ikilinganishwa na mfumo wa Video Assistant Referee (VAR).
Akizungumza kuhusu maandalizi hayo, Rais wa TFF, Wallace Karia, alisema mfumo wa Video Support utakuwa na utaratibu wa "challenge", ambapo kila kocha mkuu ataruhusiwa kuomba mapitio ya video mara nne katika kila mechi.
Kwa mujibu wa utaratibu huo, kocha atakapohisi kuna uamuzi wenye utata, atawasilisha ombi la mapitio, na mwamuzi wa kati atakwenda kwenye skrini iliyowekwa pembeni mwa uwanja kuangalia marudio kabla ya kutoa uamuzi wa mwisho. Endapo uamuzi wa awali utabadilishwa baada ya mapitio, timu haitapoteza nafasi yake ya challenge. Hata hivyo, iwapo uamuzi utabaki kama ulivyokuwa, timu itapoteza challenge moja kati ya nne ilizopewa.
TFF imeeleza kuwa sababu kuu ya kuchagua Video Support badala ya VAR ni kupunguza gharama za utekelezaji na uendeshaji. Tofauti na VAR inayohitaji kati ya kamera 12 na zaidi ya 30 pamoja na waamuzi wa video katika chumba maalumu, mfumo wa Video Support unahitaji kamera nne hadi tano pekee na hauhitaji kituo maalumu cha waamuzi wa video.
Aidha, mfumo huo unatarajiwa kuwa rahisi kufungwa katika viwanja mbalimbali nchini, ikiwemo vya mikoani, kwa kutumia miundombinu ya matangazo ya televisheni iliyopo tayari.
TFF imeeleza kuwa mchakato wa kupata idhini ya mwisho kutoka FIFA unaendelea, huku maandalizi ya majaribio yakitarajiwa kuanza katika viwanja vya Benjamin Mkapa, KMC na Azam Complex kutokana na kuwa na miundombinu inayokidhi mahitaji ya teknolojia hiyo.
Wadau wa soka wanaamini kuwa matumizi ya Video Support yatasaidia kupunguza malalamiko kuhusu maamuzi ya waamuzi, kuongeza uwazi katika uendeshaji wa mechi na kuinua hadhi ya Ligi Kuu Tanzania Bara ndani na nje ya nchi.



