Barcelona imezua mjadala mkubwa baada ya nyota wake, Lamine Yamal, kueleza wazi kuwa angefurahia kumuona mshambuliaji wa Argentina, Julián Álvarez, akijiunga na miamba hiyo ya Catalonia katika dirisha hili la usajili.
Yamal anaamini kuwa Álvarez angeendana kikamilifu na mfumo wa uchezaji wa Barcelona, akitaja uwezo wake wa kucheza nafasi mbalimbali za ushambuliaji, kufanya presha ya juu kwa wapinzani na kufunga mabao muhimu. Kwa mujibu wa winga huyo kijana, Álvarez ni aina ya mchezaji ambaye kila klabu kubwa ingetamani kuwa naye.
"Nadhani Julián Álvarez anaendana vizuri sana na mfumo wa Barcelona. Kila mtu anajua ni mchezaji mkubwa, aina ya mchezaji ambaye kila mmoja anatamani kucheza naye. Sijui hali yake ilivyo kwa sasa, lakini natumaini atajiunga nasi. Tutafurahi sana na tutampokea kwa mikono miwili," amesema Yamal.
Kauli hiyo imeongeza nguvu kwa tetesi zinazoendelea kumhusisha mshambuliaji huyo wa Argentina na Barcelona, huku mashabiki wa Blaugrana wakianza kuota ndoto za kuwaona Álvarez na Yamal wakiongoza safu ya ushambuliaji ya klabu hiyo msimu ujao.
Mtazamo wa Mwana Xtra: Ikiwa usajili huo utatimia, Julián Álvarez anaweza kuwa nyongeza kubwa kwa Barcelona kutokana na ubora wake, uwezo wa kucheza katika mifumo tofauti na uzoefu wake wa kiwango cha juu. Swali kubwa ni: Je, unaamini Álvarez ndiye mshambuliaji anayehitajika Camp Nou?