Mabingwa wa soka Tanzania Bara, Yanga SC, wameendelea na mipango yao ya kukiimarisha kikosi kuelekea msimu mpya kwa kasi ya kimya kimya, huku wakitajwa kuwa kwenye hatua za mwisho kukamilisha usajili wa walinzi wawili kutoka Mashujaa FC ya Kigoma.
Baada ya kufanya mabadiliko kwenye benchi la ufundi kwa kumtangaza kocha mkuu mpya Manqoba Mngqithi kuchukua nafasi ya Pedro Goncalves, ambaye amejiunga na AS FAR ya Morocco, Yanga sasa imeelekeza nguvu kwenye kuongeza ubora wa kikosi.
Taarifa kutoka ndani ya uongozi wa Yanga zinaeleza kuwa klabu hiyo imefikia hatua za mwisho za kukamilisha usajili wa beki wa kati Mohamed Mussa pamoja na mlinzi wa kulia Abdulnasir Gamal, wote wakiwa wanatoka Mashujaa FC.
Yanga imevamia Kigoma kuchukua vipaji
Kwa usajili huo, Yanga inaonekana kuendelea na mkakati wake wa kuimarisha kikosi kwa kuwapa nafasi wachezaji bora wanaong'ara kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara.
Mohamed Mussa anatarajiwa kuongeza nguvu kwenye eneo la ulinzi wa kati, huku Abdulnasir Gamal akitua kuziba nafasi ya Israel Mwenda, ambaye mkataba wake na Yanga umefikia mwisho.
Ukuta wa Yanga kuwa wa Watanzania
Iwapo usajili wa Mussa utakamilika rasmi, Yanga msimu ujao itakuwa na safu ya mabeki wa kati inayoundwa na wachezaji wa ndani pekee.
Mussa na Nasri Kombo wanatarajiwa kuungana na mabeki waliopo kama Ibrahim Bacca, Dickson Job na Bakari Mwamnyeto, jambo linaloonyesha dhamira ya klabu hiyo kuendelea kuamini ubora wa wachezaji wa Tanzania.
Ratiba ngumu yalazimisha kikosi kipana
Hatua hii ya Yanga inaendana na tahadhari iliyotolewa na Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Wallace Karia, ambaye alizitaka klabu kuhakikisha zinakuwa na vikosi vipana kutokana na changamoto za msimu ujao.
Ligi Kuu Tanzania Bara msimu wa 2026/27 inatarajiwa kuwa na ratiba yenye msongamano mkubwa na kumalizika mwezi Mei, hali inayoweza kusababisha timu kucheza mechi nyingi kwa vipindi vifupi.