Kombe la Dunia 2026 limeandika historia mpya baada ya timu nne zinazoshika nafasi za juu katika viwango vya FIFA kufuzu zote hatua ya nusu fainali kwa mara ya kwanza kabisa. Ufaransa , Argentina , Hispania na England zimefanikiwa kutimiza matarajio yao na sasa zinabaki hatua mbili tu kufikia ubingwa wa dunia.
Kabla ya mashindano kuanza, FIFA ilitumia mfumo wa upangaji wa makundi (seeding) uliowezesha mataifa manne yenye viwango vya juu kuepuka kukutana hadi hatua ya nusu fainali, mradi kila moja lingemaliza kileleni mwa kundi lake na kuendelea kushinda mechi za mtoano. Ndivyo ilivyotokea, na sasa dunia inajiandaa kushuhudia nusu fainali mbili zenye hadhi ya fainali.
Katika hatua hiyo, Ufaransa itamenyana na Hispania, huku Argentina ikitarajiwa kuvaana na England katika michezo inayotarajiwa kuwa miongoni mwa mikubwa zaidi kuwahi kuchezwa katika Kombe la Dunia. Kila timu ina nyota wa kiwango cha juu na historia kubwa ya mafanikio, jambo linaloongeza uzito wa pambano hilo.
Wakati huohuo, Real Madrid nayo imeendelea kutawala kwa upande wa uwakilishi wa wachezaji kwenye mashindano hayo. Nyota wanaoitumikia klabu hiyo wamechangia jumla ya mabao 19, idadi kubwa kuliko wachezaji wa klabu nyingine yoyote katika Kombe la Dunia 2026, na rekodi hiyo bado inaweza kuongezeka kabla ya mashindano kumalizika.
Kwa nyota kama Kylian Mbappé, Jude Bellingham, Vinícius Júnior na wengine wanaohusishwa na Real Madrid, mchango wao umeifanya klabu hiyo kuendelea kuonyesha ushawishi mkubwa katika soka la dunia hata wakati wa mashindano ya timu za taifa.
Kombe la Dunia 2026 sasa linaingia katika hatua zake za mwisho, huku macho ya dunia yakielekezwa kwenye pambano la kusaka tiketi ya fainali. Je, ni nani atafuzu na nani atabaki na maumivu ya kuishia nusu fainali?