Klabu ya Simba SC imemtambulisha rasmi kiungo mkabaji Kelvin Nashon kama mchezaji mpya wa kikosi hicho kwa ajili ya msimu ujao, baada ya kusaini mkataba wa miaka miwili.
Nashon anajiunga na Wekundu wa Msimbazi akiwa mchezaji huru kufuatia kumalizika kwa mkataba wake na Singida Black Stars. Msimu uliopita, kiungo huyo alicheza kwa mkopo katika klabu ya Pamba Jiji, ambapo alionyesha kiwango kizuri kilichovutia vigogo hao wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Inaelezwa kuwa Simba ilikamilisha makubaliano ya kumsajili Nashon mapema kabla ya msimu uliopita kumalizika, jambo linalomfanya kuwa miongoni mwa usajili wa kwanza wa klabu hiyo katika dirisha hili la usajili.
Usajili wa Nashon ni sehemu ya mipango ya kocha mkuu Steve Barker ya kuimarisha safu ya kiungo, hasa eneo la ukabaji. Barker anaamini kuwa uwezo wa Nashon utaongeza ushindani na uimara katikati ya uwanja, akitarajiwa kushirikiana na Yusuph Kagoma katika majukumu ya kiungo mkabaji.