Afisa Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Ligi Tanzania (TPLB), Cornel Barnabas, amesema uamuzi wa kutoa mapema ratiba ya Ligi Kuu ya NBC msimu mpya umefanyika kwa lengo la kuzipa klabu muda wa kutosha kufanya maandalizi ya kiufundi na kiutawala kabla ya kuanza kwa mashindano.
Kwa upande mwingine Barnabas amesema hatua hiyo itawezesha timu kupanga mipango yao mapema ikiwemo maandalizi ya programu za mazoezi, safari za michezo ya ugenini pamoja na mikakati ya benchi la ufundi kuelekea kila mchezo.
Pia ameongeza kwa kusema, TPLB imeendelea kuboresha mifumo ya uendeshaji wa ligi kwa kuhakikisha wadau wote wanapata taarifa muhimu kwa wakati, jambo ambalo linaongeza ufanisi na ushindani ndani ya Ligi Kuu ya NBC.
“Ratiba inapotolewa mapema, kila klabu inapata nafasi ya kupanga vizuri mambo yake. Tunataka kuona timu zinashiriki ligi zikiwa zimejiandaa kikamilifu na mashabiki nao waweze kupanga mapema kufuatilia michezo yao,” amesema Barnabas.
Kwa mujibu wa Afisa huyo, utoaji wa ratiba mapema pia unalenga kupunguza changamoto ambazo zimekuwa zikijitokeza katika misimu iliyopita, hususan upande wa maandalizi ya timu, usafiri na mipangilio ya mechi.
Ameongeza kuwa TPLB itaendelea kushirikiana na klabu, wadau wa soka pamoja na mamlaka mbalimbali kuhakikisha msimu mpya wa Ligi Kuu ya NBC unakuwa na ushindani mkubwa, uwazi na viwango bora zaidi.
Msimu mpya wa Ligi Kuu ya NBC unatarajiwa kuanza huku vilabu vikubwa nchini vikiendelea kukamilisha usajili na maandalizi ya vikosi vyao kwa ajili ya kuwania mafanikio katika mashindano ya ndani na kimataifa.