Mabingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Young Africans SC, wamemtambulisha rasmi Abdulnassir Mohamed “Gamal” kuwa mchezaji wao mpya baada ya kukamilisha usajili wake akitokea Mashujaa FC, kuelekea msimu wa 2026/27.
Gamal anawasili Jangwani akiwa mmoja wa wachezaji wenye uwezo mkubwa wa kucheza nafasi zaidi ya moja, jambo linalomfanya kuwa silaha muhimu kwa benchi la ufundi katika kupanga kikosi kulingana na mahitaji ya kila mchezo.
Nyota huyo ana uwezo wa kucheza kama beki wa kulia (Right Full Back), Wing Back, pamoja na winga, uwezo unaotarajiwa kuongeza ushindani na kumpa kocha chaguo nyingi zaidi katika safu ya pembeni.
Usajili wake ni sehemu ya maboresho yanayoendelea ndani ya kikosi cha Yanga, ambacho kinajiandaa kutetea ubingwa wa Ligi Kuu ya NBC pamoja na kufanya vizuri katika michuano ya CAF, ambapo klabu hiyo inalenga kufika mbali zaidi msimu ujao.
Mashabiki wa Wananchi sasa wanasubiri kumuona Gamal akianza rasmi maisha yake ya soka akiwa amevaa jezi ya kijani na njano, huku akitarajiwa kutumia uwezo wake wa kucheza nafasi mbalimbali kuongeza ubora na kina cha kikosi.