Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limetoa taarifa rasmi likivikumbusha vilabu kuwa zimesalia siku 25 pekee kabla ya kufungwa kwa dirisha la usajili wa msimu wa 2026/27. Dirisha hilo linahusisha vilabu vya NBC Premier League, NBC Championship League, First League, Ligi Kuu ya Vijana U-20 pamoja na Ligi Kuu ya Wanawake.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Ofisa Habari na Mawasiliano wa TFF, Cliford Mario Ndimbo, hadi kufikia Julai 21, 2026, vilabu kadhaa bado havikuwa vimesajili mchezaji hata mmoja kupitia mfumo rasmi wa FIFA Connect. Miongoni mwa vilabu vya Ligi Kuu vilivyotajwa ni Young Africans, Simba SC, Azam FC, Dodoma Jiji, JKT Tanzania, Kagera Sugar, Fountain Gate, Mashujaa FC, Mbeya City, Namungo FC, TRA United, Pamba Jiji na Polisi Tanzania.
TFF imeeleza kuwa hali hiyo pia imejitokeza katika Championship, First League na Ligi Kuu ya Wanawake, ambapo idadi kubwa ya vilabu bado haijaanza mchakato wa usajili. Shirikisho hilo limezitaka klabu zote kuhakikisha zinakamilisha usajili na uhamisho wa wachezaji kwa wakati kupitia mfumo wa FIFA Connect.
Aidha, TFF imesisitiza kuwa hakutakuwa na nyongeza ya muda wa dirisha la usajili, hivyo vilabu vinapaswa kutumia siku zilizobaki kukamilisha taratibu zote muhimu. Hatua hiyo inalenga kuhakikisha maandalizi ya msimu mpya yanafanyika kwa wakati na kwa kuzingatia kanuni za usajili zilizowekwa.