Manchester City imeendelea kuonyesha imani kubwa kwa nyota wake wa kimataifa wa England, Phil Foden, baada ya kiungo huyo mshambuliaji kusaini mkataba mpya utakaomuweka Etihad Stadium hadi mwaka 2030.
Foden, ambaye amepitia akademi ya Manchester City tangu akiwa mtoto, ameamua kuendelea na safari yake katika klabu hiyo licha ya kuwa na kipindi cha changamoto za kiwango na ushindani mkubwa ndani ya kikosi. Mkataba huo mpya unatajwa kuwa wa miaka minne zaidi, huku kukiwa na kipengele cha kuongeza mwaka mmoja zaidi.
Nyota huyo mwenye umri wa miaka 26 amekuwa mmoja wa wachezaji muhimu zaidi katika historia ya kizazi kipya cha Manchester City. Tangu alipopandishwa kwenye kikosi cha wakubwa, Foden ameshinda mataji mbalimbali ikiwemo Ligi Kuu England, Ligi ya Mabingwa Ulaya na vikombe vingine vya ndani.
Uamuzi wa Manchester City kumpa mkataba mpya Foden unaonyesha mpango wa klabu hiyo kuendelea kujenga kikosi chake kwa kuwategemea wachezaji waliotoka ndani ya mfumo wake wa akademi.
Foden amekuwa sehemu ya kizazi cha wachezaji waliothibitisha uwezo wao kutoka akademi ya City, sambamba na wachezaji wengine kama Rico Lewis ambaye pia aliongezewa mkataba hadi 2030.
Ingawa msimu uliopita haukuwa rahisi kwake kutokana na ushindani wa nafasi na changamoto za majeraha, uongozi wa Manchester City unaamini bado ana uwezo mkubwa wa kurejea kwenye kiwango chake bora.
Mchezaji huyo amesisitiza furaha yake ya kuendelea kubaki katika klabu ambayo ameikulia na ambayo ameitumikia tangu akiwa kijana.