Saa chache baada ya Klabu ya Simba SC kutangaza kufikia makubaliano ya kumuongezea mkataba wa mkopo mshambuliaji Selemani Mwalimu, Wydad Athletic Club (Wydad AC), wameibuka na kukanusha taarifa hizo huku wakitishia kuchukua hatua kali za kisheria.
Katika taarifa rasmi iliyotolewa na Wydad kupitia kurasa zao za kijamii, miamba hiyo ya Casablanca imebainisha kuwa hakuna makubaliano yoyote yaliyofikiwa kati yao na Simba kuhusu mchezaji huyo, na kwamba taarifa zilizosambazwa na si za kweli.
Wydad imesisitiza kuwa Selemani Mwalimu bado ni mchezaji wao halali kisheria na yumo kwenye mipango ya benchi la ufundi kwa ajili ya msimu ujao, hivyo anapaswa kurejea kikosini haraka iwezekanavyo.
"Uongozi wa Wydad Athletic Club unapenda kuufahamisha umma na mashabiki kuwa taarifa zinazosambazwa na Klabu ya Simba kuhusu makubaliano mapya ya Selemani Mwalimu si za kweli. Hatujasaini mkataba wowote na klabu hiyo," ilieleza sehemu ya taarifa ya miamba hiyo ya Morocco.
Aidha, Wydad imeongeza kuwa itawasilisha malalamiko rasmi kwenye Shirikisho la Mpira wa Miguu Duniani (FIFA) pamoja na Shirikisho la Soka Afrika (CAF) dhidi ya Simba SC kwa kile walichokiita ni ukiukwaji wa taratibu za usajili na upotoshaji wa makusudi unaolenga kuchafua taswira ya klabu hiyo.