Waamuzi wa Ligi Kuu Tanzania Bara wameingia katika awamu ya tano ya mafunzo ya matumizi ya teknolojia ya Video Assistant Referee (VAR), ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kuelekea matumizi rasmi ya mfumo huo katika soka la Tanzania. Mafunzo hayo yanaendelea chini ya usimamizi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), likiongozwa na Rais wake, Wallace Karia.
Mafunzo hayo yanalenga kuwajengea waamuzi uwezo wa kutumia mfumo wa VAR kwa ufanisi, ikiwemo kufanya maamuzi sahihi katika matukio muhimu kama mabao, mikwaju ya penalti, kadi nyekundu na makosa ya utambulisho wa wachezaji. Washiriki pia wanaendelea na mafunzo ya vitendo yanayohusisha mawasiliano kati ya waamuzi wa uwanjani na waamuzi waliopo kwenye chumba cha VAR.
Hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa TFF wa kuboresha kiwango cha uamuzi nchini na kuendana na viwango vya kimataifa vya usimamizi wa soka. Inatarajiwa kuwa matumizi ya VAR yatasaidia kupunguza makosa ya uamuzi, kuongeza uwazi katika mechi za Ligi Kuu Tanzania Bara na kuimarisha imani ya vilabu, wachezaji na mashabiki kwa waamuzi wa ndani