Klabu ya Zamalek ya Misri imepiga hatua kubwa katika jitihada za kuondolewa marufuku ya usajili iliyowekwa na Shirikisho la Soka Duniani (FIFA), baada ya kupunguza idadi ya kesi za kifedha zinazoikabili kutoka 18 hadi tano. Hatua hiyo imekuja kufuatia klabu hiyo kufanikiwa kumaliza migogoro kadhaa iliyokuwa ikihusisha madeni ya wachezaji, makocha wa zamani na vilabu mbalimbali.
Awali, Zamalek ilikuwa ikikabiliwa na zaidi ya kesi 17 zilizohitaji kulipwa zaidi ya dola milioni 6.17 za Marekani ili kuondoa vikwazo hivyo. Hata hivyo, uongozi wa klabu umeendelea kutatua migogoro hiyo hatua kwa hatua, na sasa umebakiza kesi tano pekee kabla ya kufikia uhuru kamili wa kufanya usajili.
Endapo Zamalek itafanikiwa kumaliza kesi zilizobaki, FIFA itaiondoa rasmi marufuku hiyo na kuiruhusu kusajili wachezaji wapya kuelekea msimu wa 2026/27. Hatua hiyo pia itaongeza nafasi ya klabu hiyo kujiandaa vyema kwa mashindano ya ndani na yale ya CAF, huku mashabiki wakisubiri kwa matumaini kurejea kwa Zamalek katika ushindani wa juu.