Klabu ya St Eloi Lupopo ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) imethibitisha rasmi kuwa itafanya kambi yake ya maandalizi ya msimu mpya (pre-season) nchini Tanzania.
Mabingwa hao wa Congo wanatarajiwa kuweka kambi kwa siku kadhaa wakijiandaa na msimu wa 2026/27, huku Tanzania ikichaguliwa kutokana na mazingira mazuri ya maandalizi pamoja na ushindani wa vilabu vya Ligi Kuu Tanzania Bara.
Taarifa zinaeleza kuwa Lupopo inapanga kuomba kucheza mechi kadhaa za kirafiki dhidi ya baadhi ya timu imara nchini, huku Young Africans SC ikitajwa kuwa miongoni mwa wapinzani wanaolengwa kwa ajili ya michezo hiyo ya majaribio.
Iwapo mechi hiyo itathibitishwa, itakuwa fursa muhimu kwa Yanga na St Eloi Lupopo kupima vikosi vyao kabla ya kuanza kwa mashindano rasmi, sambamba na kuwapa makocha nafasi ya kutathmini wachezaji wapya na mifumo ya uchezaji.
Kwa Yanga, mchezo wa kirafiki dhidi ya Lupopo unaweza kuwa sehemu muhimu ya maandalizi kuelekea Ligi Kuu Tanzania Bara na Ligi ya Mabingwa Afrika, huku kwa Lupopo ukiwa mtihani wa kujiandaa kwa msimu mpya wa mashindano nchini DR Congo.