Pazia la michuano ya Kombe la Mataifa ya Wanawake Afrika (WAFCON 2026) linafunguliwa rasmi nchini Morocco, huku mataifa 16 yakijiandaa kuwania taji la ubingwa wa Afrika kwa upande wa wanawake.
Michuano hiyo inatarajiwa kuwa na ushindani mkubwa kutokana na uwepo wa timu zenye historia na ubora mkubwa katika soka la wanawake barani Afrika, huku macho yakiwa kwa mabingwa watetezi, wenyeji Morocco pamoja na mataifa mengine yenye nguvu kama Nigeria, Afrika Kusini, Zambia, Ghana na Cameroon.
Katika ratiba ya hatua ya makundi, Algeria itaanza kampeni dhidi ya Senegal siku ya Jumapili Julai 26 saa 2:00 usiku, kabla ya wenyeji Morocco kushuka dimbani dhidi ya Kenya saa 5:00 usiku.
Timu ya taifa ya Tanzania, Twiga Stars, itaanza safari yake ya kusaka mafanikio katika michuano hiyo Jumatatu Julai 27 dhidi ya Afrika Kusini, mchezo unaotarajiwa kuwa na ushindani mkubwa kutokana na ubora wa timu zote mbili.
Mbali na mchezo huo, Ivory Coast itakutana na Burkina Faso katika siku hiyo hiyo, huku siku zinazofuata mashabiki wakitarajia kuona michezo mingine mikubwa ikiwemo Zambia dhidi ya Misri, Nigeria dhidi ya Malawi, Ghana dhidi ya Cape Verde pamoja na Cameroon dhidi ya Mali.
Michuano hiyo pia itashuhudia mechi kubwa katika hatua ya makundi, ikiwemo Senegal dhidi ya Kenya na Morocco dhidi ya Algeria, huku kila timu ikipambana kupata nafasi ya kufuzu hatua inayofuata.
WAFCON 2026 imeendelea kuwa jukwaa muhimu la kukuza soka la wanawake Afrika, huku wachezaji wakitumia michuano hiyo kuonyesha vipaji vyao na kuwania nafasi za kuwakilisha nchi zao katika mashindano makubwa ya kimataifa.
Kwa Tanzania, matumaini makubwa yanaelekezwa kwa Twiga Stars kuhakikisha wanafanya vizuri dhidi ya wapinzani wao na kuandika historia mpya katika michuano hiyo ya wanawake Afrika.