Shirikisho la Soka la Ufaransa (FFF) limemtangaza rasmi Zinedine Zidane kuwa kocha mkuu mpya wa Timu ya Taifa ya Ufaransa, akichukua nafasi ya Didier Deschamps aliyehitimisha kipindi chake cha miaka 14 madarakani. Zidane amesaini mkataba wa miaka minne utakaomuweka madarakani hadi kampeni ya Kombe la Dunia 2030.
Uteuzi wa Zidane unakuja baada ya kujijengea sifa kubwa akiwa kocha wa Real Madrid, alikoiongoza klabu hiyo kutwaa mataji matatu mfululizo ya Ligi ya Mabingwa Ulaya kati ya mwaka 2016 na 2018, pamoja na ubingwa wa La Liga msimu wa 2019/20. Mafanikio hayo yamemfanya kuwa mmoja wa makocha wenye heshima kubwa katika soka la dunia.
Zidane anarithi mikoba ya Didier Deschamps, ambaye aliiongoza Ufaransa kutwaa Kombe la Dunia mwaka 2018, kufika fainali ya Kombe la Dunia 2022 na Euro 2016. Hata hivyo, safari yake ilifikia mwisho baada ya Ufaransa kutolewa katika nusu fainali ya Kombe la Dunia 2026 na baadaye kupoteza mchezo wa kutafuta mshindi wa tatu.
Akiwa mmoja wa wachezaji wakubwa katika historia ya Ufaransa, Zidane aliiongoza Les Bleus kutwaa Kombe la Dunia mwaka 1998 na Kombe la Mataifa ya Ulaya mwaka 2000. Sasa anaanza sura mpya akiwa kocha mkuu, akipewa jukumu la kuirejesha Ufaransa kwenye mafanikio makubwa ya kimataifa, huku mechi yake ya kwanza ikitarajiwa kuwa dhidi ya Uturuki katika Ligi ya Mataifa ya UEFA.