Huenda mashabiki wa Yanga leo wakapata nafasi ya kumshuhudia mshambuliaji wao mpya, Seleman Mwalimu, akicheza kwa mara ya kwanza katika kikosi hicho kwenye mchezo wa Ligi Kuu ya Tanzania dhidi ya Pamba Jiji.
Yanga itakuwa mwenyeji wa Pamba Jiji leo Ijumaa, Agosti 28, katika mchezo utakaopigwa saa 3:00 usiku kwenye Uwanja wa KMC Complex.
Mwalimu, ambaye usajili wake uliibua gumzo wakati wa dirisha la usajili baada ya Yanga kumnasa kutoka kwenye kambi ya watani wao, Simba SC, alikuwa hajaanza kuitumikia timu hiyo kutokana na kusubiriwa kwa hati yake ya kimataifa ya uhamisho wa mchezaji (ITC).
Hata hivyo, taarifa zinaeleza kuwa suala hilo sasa limepata ufumbuzi baada ya Shirikisho la Soka la Morocco (FRMF) kutuma ITC ya mshambuliaji huyo kwa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), hatua inayomuweka katika nafasi ya kuanza kuitumikia Yanga.
Iwapo kocha Manqoba Mngqithi ataamua kumtumia, Mwalimu anaweza kuonekana uwanjani leo dhidi ya Pamba Jiji, huku mashabiki wa Yanga wakisubiri kwa hamu kumuona mchezaji huyo mpya akianza safari yake rasmi katika klabu hiyo.
Tofauti na Stephane Aziz Ki, ambaye Mngqithi alisema bado hajawa tayari kucheza, Mwalimu anaonekana kuwa katika nafasi nzuri zaidi kwa kuwa amepata muda wa kutosha wa kufanya mazoezi na timu.
Kabla ya kusajiliwa na Yanga, Mwalimu alikuwa sehemu ya maandalizi ya msimu mpya katika kambi za Simba na Wydad Casablanca, hivyo tayari alikuwa katika programu za mazoezi ya kabla ya msimu (pre-season).



