Kocha Mkuu wa Simba, Steve Barker, amemtetea mshambuliaji Ibrahim Doumbia baada ya kukosa kutumia baadhi ya nafasi alizopata katika mchezo dhidi ya Coastal Union, akisisitiza kuwa hana wasiwasi na uwezo wa nyota huyo kufunga mabao mengi msimu huu.
Simba ilipata ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Coastal Union katika mchezo uliopigwa kwenye Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, huku Doumbia akipata nafasi kadhaa za kufunga lakini akashindwa kuzitumia ipasavyo.
Licha ya kutofunga, Barker amesema mshambuliaji huyo alifanya kazi kubwa uwanjani na kwamba alikosa bahati ya kuweka mpira kambani.
“Doumbia ni mshambuliaji mzuri, sisi tunamuamini. Nafikiri leo alikosa bahati tu ya kufunga, lakini amefanya jitihada kubwa uwanjani,” alisema Barker.
Kocha huyo ameongeza kuwa hali hiyo ni ya kawaida kwa mchezaji mpya, akieleza kuwa Doumbia bado anahitaji muda wa kuzoea mazingira mapya pamoja na mfumo wa uchezaji wa Simba.
“Hii ni hali ya kawaida kwa mchezaji mgeni. Anahitaji kuzoea mazingira pamoja na mfumo wetu wa uchezaji kwa ujumla.”
Barker amesema hana mashaka na uwezo wa mshambuliaji huyo na anaamini muda si mrefu ataanza kuonyesha makali yake mbele ya lango.
“Sina wasiwasi naye, ni mchezaji mzuri. Ninaamini atatufungia mabao mengi msimu huu,” alisema Barker.
Wakati huo huo, mashabiki wa Simba wamehimizwa kuendelea kumpa Doumbia sapoti na kumvumilia katika kipindi hiki cha mwanzo, ili kumpunguzia presha na kumpa nafasi ya kuzoea mazingira na mfumo wa timu.



