Aston Villa imekamilisha dili la kumsajili winga wa kimataifa wa Ureno, Rafael Leão, kutoka AC Milan kwa mkopo. Kwa mujibu wa taarifa hiyo, makubaliano yamefikia hatua ya mwisho na nyaraka zote za uhamisho tayari zimekamilishwa, hivyo Leão sasa anajiandaa kuanza ukurasa mpya wa maisha yake ya soka akiwa England.
Katika dili hilo, Aston Villa imepata nafasi ya kumnunua moja kwa moja Leão kupitia kipengele cha buy option chenye thamani ya takribani pauni milioni 41. Hii inamaanisha kuwa baada ya kipindi cha mkopo, Villa inaweza kutumia fursa hiyo kumsajili mshambuliaji huyo kwa mkataba wa kudumu iwapo atafanya vizuri na klabu ikaamua kuendelea naye.
Aston Villa pia imekubali kubeba mshahara wa Leão unaokadiriwa kufikia euro milioni 8 kwa mwaka. Kocha Unai Emery ametajwa kuwa mtu muhimu katika kufanikisha uhamisho huo, akiongoza kwa karibu jitihada za klabu hiyo kumpata winga huyo ambaye anajulikana kwa kasi, uwezo wa kupiga chenga na kutengeneza nafasi pamoja na kufunga mabao.
Kwa Aston Villa, ujio wa Leão ni nyongeza kubwa katika safu ya ushambuliaji na unaonyesha wazi dhamira ya klabu hiyo kujenga kikosi chenye ushindani zaidi. Kwa upande wa Leão, uhamisho huu unampa nafasi ya kujaribu changamoto mpya katika Premier League baada ya kipindi chake AC Milan. Sasa macho yote yatakuwa kwake kuona kama ataweza kuonyesha kiwango kikubwa ndani ya kikosi cha Unai Emery na hatimaye kuifanya Aston Villa iamue kutumia pauni milioni 41 kumnunua moja kwa moja.



