Kocha Mkuu wa Yanga, Manqoba Mngqithi, amewaomba mashabiki wa timu hiyo mkoani Arusha kujitokeza kwa wingi katika Uwanja wa Sheikh Amri Abeid kesho Jumatatu, huku akisisitiza umuhimu wa kuibuka na ushindi dhidi ya Fountain Gate.
Yanga itakuwa ugenini kesho Jumatatu majira ya saa 10 jioni kuikabili Fountain Gate katika mchezo wa raundi ya tano ya Ligi Kuu, huku kikosi hicho kikilenga kuendeleza mwenendo wake mzuri katika mashindano hayo.
Akizungumza na wanahabari leo kuelekea mchezo huo, Mngqithi amesema anatarajia kukutana na changamoto kubwa kutokana na ubora wa Fountain Gate, pamoja na uwepo wa kocha Fredy Minziro ambaye anaifahamu vizuri Yanga.
Mngqithi amesisitiza kuwa Yanga haitafanya kosa la kumdharau mpinzani wake kwa sababu tu hajapata ushindi katika michezo iliyopita, akieleza kuwa Fountain Gate ina kikosi chenye ushindani.
“Hizi ni miongoni mwa mechi ngumu na ni muhimu sana kushinda. Tunafahamu Fountain Gate wana mwalimu mzuri ambaye amewahi kuwa sehemu ya benchi la Yanga, hivyo anajua tamaduni za klabu. Ni mzoefu na ana wachezaji wazuri. Sisi kama Yanga tunapaswa kufanya kazi kubwa ili kushinda kesho,” alisema Mngqithi.
Kocha huyo wa Yanga amesema wamefanya uchambuzi wa namna Fountain Gate inavyocheza na kwamba maandalizi ya mwisho yanaendelea kabla ya mchezo huo.
“Tunafahamu wapinzani wetu wamepoteza michezo kadhaa hapo nyuma, lakini jukumu letu ni kuheshimu kila mchezo. Tumewaangalia Fountain Gate namna wanavyocheza na leo tunakwenda kufanya maandalizi ya mwisho ya kucheza nao. Naamimi tutakuwa na mechi nzuri,” aliongeza.
Mngqithi awaomba Wananchi kujaa Sheikh Amri Abeid
Mbali na maandalizi ya kiufundi, Mngqithi ametumia nafasi hiyo kuwaomba mashabiki wa Yanga, maarufu kama Wananchi, kujitokeza kwa wingi uwanjani ili kuipa timu hamasa katika mchezo huo.
Kocha huyo amesema uwepo wa mashabiki ni muhimu kwake na kwa wachezaji, akieleza kuwa sapoti yao humuongezea morali ya kufanya vizuri.
“Nawaomba sana Wananchi waje kwa wingi. Wao ni muhimu sana kwa timu, ni muhimu pia kwangu kama kocha kwa sababu wananipa morali ya kufanya vyema kila siku. Nawashukuru sana kwa sapoti yao tangu tumefika hapa nchini na nawaomba kesho waje ili tushinde pamoja,” alisema Manqoba.
Mchezo huo unatarajiwa kuwa kipimo kingine kwa Yanga katika harakati zake za kuendeleza ubabe wake kwenye Ligi Kuu, huku Fountain Gate ikiwa na jukumu la kuzuia kasi ya mabingwa hao.



