Barcelona imefikia makubaliano ya kushtukiza na Arsenal kwa ajili ya kumsajili mshambuliaji wa Brazil, Gabriel Jesus.
Jesus, mwenye umri wa miaka 29, anatarajiwa kusafiri kwenda Hispania mapema wiki hii kwa ajili ya vipimo vya afya, huku Arsenal ikiwa tayari imemruhusu kusafiri ili kukamilisha taratibu za uhamisho huo.
Barcelona inatarajiwa kulipa kiasi cha €10 milioni pamoja na nyongeza ili kumpata mshambuliaji huyo, ada ambayo ni ndogo ikilinganishwa na thamani yake ya soko inayokadiriwa kuwa kati ya €16 milioni na €17 milioni.
Usajili huo unakuja baada ya siku kadhaa za sintofahamu kuhusu mustakabali wa Jesus huko Arsenal, ambapo mshambuliaji huyo alikuwa nje ya mazoezi ya kikosi cha kwanza na alitarajiwa kuondoka klabuni hapo kabla ya kufungwa kwa dirisha la usajili.
Kwa mujibu wa Mundo Deportivo, usajili huo ulisukumwa na Mkurugenzi wa Michezo wa Barcelona, Deco, huku klabu hiyo ikitarajia kukamilisha dili hilo ndani ya saa 24 zijazo.



