Raja Casablanca imeingia kwenye sintofahamu baada ya Kocha Mkuu wa klabu hiyo, Nasreddine Nabi, kuondoka jijini Casablanca na kuelekea Brussels, huku taarifa zikieleza kuwa kuna mvutano ndani ya uongozi wa klabu hiyo.
Chanzo kikuu cha mvutano huo kinatajwa kuwa tofauti za kiutendaji kati ya Nabi na Mkurugenzi wa Michezo wa klabu hiyo, hasa kuhusu masuala ya usajili. Nabi alitarajiwa kuwa na ushawishi katika maamuzi ya usajili baada ya kuteuliwa kuwa kocha, lakini inadaiwa mkurugenzi huyo amekuwa akitaka kuwa na udhibiti mkubwa katika mchakato huo.
Miongoni mwa matukio yaliyoongeza mvutano ni suala la usajili wa Maseko, ambaye Nabi alidaiwa kuwasiliana naye akiwa bado Mamelodi Sundowns na kufikia makubaliano ya awali. Hata hivyo, mpango huo baadaye ulipingwa na Mkurugenzi wa Michezo, jambo lililomfanya Nabi kutoridhishwa na mwenendo wa klabu.
Taarifa hizo pia zinadai kuwa Mkurugenzi wa Michezo huyo alikuwa ameanza mazungumzo na kocha mwingine takribani wiki tatu zilizopita, wakati Nabi bado akiwa kazini. Hali hiyo imeongeza maswali kuhusu mustakabali wa Nabi na namna klabu hiyo inavyoendeshwa, huku mashabiki wakisubiri hatua itakayofuata kutoka kwa uongozi wa Raja Casablanca.



