Mashabiki wa CAF Champions League na CAF Confederation Cup wameelekezwa kufahamu kuwa katika duru za awali za mashindano hayo, urushaji wa moja kwa moja wa mechi hauko chini ya usimamizi wa CAF, bali jukumu hilo linabebwa na timu mwenyeji.
Kwa mujibu wa utaratibu huo, timu mwenyeji inawajibika kufanya makubaliano na kituo cha televisheni au mtangazaji kwa ajili ya kurusha mchezo. Hivyo, baadhi ya mechi zinaweza kuonyeshwa moja kwa moja huku nyingine zikikumbwa na changamoto za kutorushwa au ubora wa picha na mtandao.
Wadau wa soka wamewataka mashabiki kuelewa hali hiyo, hususani kuelekea mechi za wikendi hii, kwa kuwa endapo mchezo wa klabu yao hautarushwa moja kwa moja au ukawa na changamoto za ubora wa matangazo, suala hilo linapaswa kuhusishwa na timu mwenyeji katika hatua hiyo ya mashindano.
Hata hivyo, kuanzia hatua ya makundi na hatua zinazofuata, CAF itakuwa na jukumu la kusimamia urushaji wa mechi, hatua inayolenga kuweka mfumo mmoja wa matangazo na kupunguza changamoto zinazoweza kujitokeza katika duru za awali.



