Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limetangaza kikosi cha awali cha Timu ya Taifa, Taifa Stars, kwa ajili ya michezo ya kufuzu Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2027 dhidi ya Guinea-Bissau na Madagascar, pamoja na mchezo wa kirafiki dhidi ya Ghana.
Kikosi hicho kilichoandaliwa na Kocha Mkuu Miguel Ángel Gamondi kinajumuisha makipa watano, akiwemo Zuberi Foba na Aishi Manula wa Azam FC. Katika safu ya ulinzi, wamejumuishwa Ibrahim Bacca na Bakari Mwamnyeto wa Yanga SC, pamoja na Vedastus Masinde na Bakari Msimu wa Simba SC.
Safu ya kiungo imejumuisha wachezaji wanaocheza nje ya Tanzania, akiwemo Adolph Mtasingwa wa Kaizer Chiefs, Mohamed Sagaf wa Eastbourne Borough na Alphonce Mabula wa JS Kabylie, sambamba na wachezaji kutoka klabu za ndani. Upande wa ushambuliaji, majina yanayokamilisha kikosi hicho ni pamoja na Bernard Kamungo, Kelvin John, Kibu Dennis na Cyprian Kachwele, huku Selemani Mwalimu na Paul Peter wakiwakilisha ligi ya ndani.




