Mchezaji wa Kimataifa wa timu ya Taifa ya Wanawake ya Tanzania, Clara Luvanga, ameandika historia mpya katika soka la wanawake baada ya kukamilisha uhamisho wake kutoka Al-Nassr ya Saudi Arabia kwenda Washington Spirit ya Marekani.
Luvanga amesaini mkataba wa miaka minne utakaomuweka Washington Spirit hadi mwaka 2029, katika usajili unaoelezwa kuwa na thamani ya takribani dola milioni 2.3(zaidi ya Tsh 6B)
Kiasi hicho kinatajwa kuwa ada kubwa zaidi ya uhamisho kuwahi kulipwa kwa mchezaji wa soka la wanawake, hivyo kumweka Luvanga katika ukurasa mpya wa historia ya soka la wanawake duniani.
Rekodi mpya kwa Tanzania
Uhamisho huo pia unampa Luvanga heshima ya kuwa Mtanzania wa kwanza kucheza katika historia ya National Women’s Soccer League (NWSL) nchini Marekani.
Hatua hiyo ni mafanikio makubwa kwa Luvanga binafsi na Tanzania kwa ujumla, huku akizidi kuiweka nchi kwenye ramani ya soka la wanawake duniani.
Safari ya Luvanga imekuwa ya kuvutia, kuanzia Yanga Princess, akipiga hatua hadi soka la Hispania, kisha kujiunga na Al-Nassr nchini Saudi Arabia na sasa kuhamia Marekani.