Kocha wa muda wa Timu ya Taifa ya Zambia, George Lwandamina, ametangaza kikosi cha wachezaji 27 kwa ajili ya michezo miwili ya kufuzu AFCON 2027, huku mshambuliaji wa Yanga SC, Albert Kangwanda, akiwa miongoni mwa walioitwa katika kikosi hicho.
Zambia itaanza kampeni hizo kwa kucheza dhidi ya Algeria ugenini Septemba 25, 2026, kabla ya kurejea nyumbani Septemba 29 kukabiliana na Togo katika Uwanja wa Levy Mwanawasa, Ndola. Zambia ipo Kundi I pamoja na Algeria, Togo na Burundi.
Kangwanda amejumuishwa katika safu ya washambuliaji pamoja na nyota wengine kama Patson Daka wa Hamburg, Fashion Sakala wa Al Fayha na Kingston Mutandwa wa Servette.
Kwa Kangwanda, wito huo unampa nafasi ya kuendelea kuiwakilisha Zambia katika hatua ya kimataifa, huku akiwa mmoja wa wachezaji wanaotarajiwa kusaidia Chipolopolo katika harakati za kuwania nafasi ya kushiriki AFCON 2027, ambayo itaandaliwa kwa pamoja na Tanzania, Kenya na Uganda.