Mamelodi Sundowns imeandika ushindi muhimu kwenye mashindano ya FIFA Intercontinental Cup 2026 baada ya kuichapa Al Ahli ya Saudi Arabia kwa mabao 2-1 katika mchezo uliopigwa Jumamosi, Septemba 19, 2026, kwenye Uwanja wa Loftus Versfeld.
Shujaa wa mchezo alikuwa mshambuliaji wa Sundowns, Nuno Santos, aliyefunga mabao yote mawili ya timu yake na kuiwezesha klabu hiyo ya Afrika Kusini kusonga mbele katika mashindano hayo.
Sundowns ilianza kwa kasi na kupata bao la kwanza dakika ya 17, Santos akimalizia kwa kichwa mpira uliopigwa na Teboho Mokoena na kuipa timu yake uongozi wa 1-0.
Hata hivyo, furaha ya wenyeji haikudumu kwa muda mrefu. Dakika mbili baadaye, Al Ahli ilisawazisha baada ya shuti la Feras Al Brikan kumgonga kipa Ronwen Williams na mpira kuingia wavuni kwa kujifunga.
Kipindi cha pili kilikuwa cha ushindani mkubwa huku timu zote zikisaka bao la ushindi. Sundowns hatimaye ilipata kile ilichokitafuta dakika ya 80, Santos akifunga tena kwa kichwa na kuifanya timu yake kuongoza 2-1. Bao hilo liliamua mchezo.
Ushindi huo umeifanya Sundowns kutwaa FIFA African-Asian-Pacific Cup na kusonga mbele kwenye hatua inayofuata ya FIFA Intercontinental Cup.
Sundowns sasa itakutana na mshindi wa Derby of the Americas, ambao utawakutanisha Toluca ya Mexico na mshindi wa Copa Libertadores ya mwaka 2026.
Mshindi wa hatua hiyo ataendelea kwenye FIFA Challenger Cup, ambapo nafasi ya kufuzu kwa fainali dhidi ya mabingwa wa Ulaya, Paris Saint-Germain, itakuwa kwenye mstari.
Kwa ushindi huu, Mamelodi Sundowns imeonyesha kuwa mabingwa wa Afrika wako tayari kushindana katika jukwaa la dunia, huku Nuno Santos akichukua nafasi ya shujaa wa siku kwa mabao yake mawili yaliyowapa Wabrazilians ushindi muhimu.