Katibu Mkuu wa Ihefu, Zagalo Chalamila amesema uamuzi wa timu hiyo kumtangaza kocha mkongwe John Simkoko kuwa Kocha Mkuu umetokana na kocha wao Zubery Katwila kukosa sifa za kukaa kwenye benchi
Zagalo amesema baada ya kuondoka kwa Juma Mwambusi walipewa nafasi ya Katwila kuongoza kati ya michezo minne hadi mitano, na baada ya hapo walitakiwa kutafuta kocha mwenye vigezo vinavyotakiwa.
"Wengi wanadhani Katwila hatumuamini, lakini wanashindwa kuelewa ana leseni 'B' na ili ukae katika benchi unatakiwa uwe na 'A' ya CAF, ndiyo maana unaona amerudi darasani kusoma," alisema
Zagalo alisema wana matumaini makubwa na ushirikiano uliopo baina ya Katwila na Simkoko huku akiweka wazi uzoefu wake utakuwa na manufaa makubwa katika kikosi chao ambacho kimekuwa na matokeo mazuri kwa sasa.



