Baada ya kukubali kichapo cha pili kwenye hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika, wawakilishi wa Tanzania, Klabu ya Simba, sasa matarajio yao pekee ya kutinga robo fainali ya michuano hiyo ni yatategemea makosa ya wapinzani wake pia
Simba ambayo imekuwa na rekodi nzuri ya ushindi inapocheza katika Uwanja wa Benjamin Mkapa kwenye michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika, juzi ilikubali kichapo cha mabao 3-0 uwanjani hapo dhidi ya Raja Casablanca ya Morocco, hicho kikiwa kipigo cha pili katika hatua hiyo baada ya mechi ya awali ugenini nchini Guinea kuchapwa bao 1-0 dhidi ya Horoya AC.
Lakini kipigo hicho katika Uwanja wa Benjamin Mkapa kwa Simba ni cha kwanza kwao katika hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika kufungwa uwanjani hapo katika ushiriki wake wote wa michuano hiyo.
Matokeo hayo yanaifanya Raja Casablanca kuongoza Kundi C kwa kuwa na pointi sita, ikifuatiwa na Horoya AC yenye alama nne na Vipers ya Uganda ikishika nafasi ya tatu kwa pointi yake moja huku Simba ikiburuza mkia bila pointi yoyote.
Kwa maana hiyo, ili Simba iweze kutinga hatua ya robo fainali inapaswa kushinda michezo yake mitatu ijayo dhidi ya Vipers ugenini na nyumbani na kisha itapaoikaribisha Horoya AC hapa nchini, lakini kuiombea mema Raja Casablaca ishinde michezo yake mitatu ijayo kabla ya kuhitimisha kwa kukutana na Wekundu wa Msimbazi hao.
Hii ina maana kama Simba ikishinda mechi zake tatu kabla ya kuhitimisha dhidi ya Raja Casablaca, itafikisha pointi tisa, huku miamba hiyo ya Morocco ikishinda tu dhidi ya Horoya nyumbani na ugenini, itakuwa imefikisha pointi 12, wakati mabingwa hao wa Guinea watabaki na alama zao nne kabla ya kufunga hatua ya makundi dhidi ya Vipers.
Hivyo, hata kama Horoya itashinda dhidi ya Vipers na kutoka sare mechi moja dhidi ya Raja Casablanca ina maana itamaliza na pointi nane, moja nyuma ya Simba ambayo haipewi nafasi kubwa ya kwenda kuambulia hata sare ugenini dhidi ya miamba hiyo ya Morocco



