Beki wa kulia wa Simba Shomari Kapombe amesema ni heshima kubwa kwa wachezaji na klabu ya Simba kwa ujumla kupata nafasi ya kushiriki michuano ya African Football League (Super League) ambayo inafanyika kwa mara ya kwanza barani Afrika
Simba ni miongoni mwa timu nane zilizopata nafasi hiyo baada ya kufanya vizuri kwenye michuano ya CAF katika miaka mitano iliyopita
Baada ya droo ya mechi za robo fainali kufanyika na Simba kupangwa kucheza na Al Ahly, Kapombe amesema hawana hofu yoyote juu ya kuwakabili Al Ahly kwani wana rekodi nzuri wanapokutana nyumbani na wababe hao wa soka la Afrika
"Kwanza ni heshima kubwa kwetu wachezaji na klabu ya Simba kupata nafasi ya kuwa miongoni mwa timu nane kubwa barani Afrika kushiriki mashindano haya kwa mara ya kwanza"
"Mechi dhidi ya Al Ahly itakuwa nzuri, katika uwanja wa Benjamin Mkapa historia yetu ni nzuri tunapokutana na Al Ahly, tumeweza kuwafunga mara zote"
"Sisi kama Simba tunajiandaa kufanya vizuri ili tusonge mbele katika mashindano hayo," alisema Kapombe
Kapombe ni mmoja wa wachezaji ambao walikuwemo katika vikosi vya Simba vilivyopata ushindi katika mechi zote dhidi ya Al Ahly katika uwanja wa Benjamin Mkapa
Wachezaji wengine ni Aishi Manula, Clatous Chama, Mohammed Hussein, nahodha John Bocco, Mzamiru Yassin na Luis Miquissone ambaye alifunga bao la ushindi katika mchezo wa mwisho uliozikutanisha timu hizo uwanja wa Benjamin Mkapa



