Wenyewe wanaiita Pacha Derby! Ni siku ya Ijumaa Oktoba 25 nyasi za uwanja wa CCM Liti mkoani Singida zitawaka moto pale timu 'mapacha' Singida Black Stars na Fountain Gate zitakapoumana
Hii itakuwa mechi ya aina yake ambayo itazikutanisha timu mbili bora katika ligi kuu ya NBC msimu huu
Singida BS iko kileleni mwa msimamo wa ligi ikikusanya alama 19 baada ya mechi 7 wakati Fountain Gate wako nafasi ya nne wakiwa na alama 16 baada ya mechi 8
Upinzani wa timu hizi ulianza msimu uliopita pale baadhi ya waliokuwa mabosi wa Singida Big Stars kujitoa na kuinunua Ihefu Fc huku wakiondoka na karibu nyota wote wa kigeni waliokuwa wakiitumikia timu hiyo
Baadae Ihefu Fc ikabadili jina na kuitwa Singida Black Stars huku ikihamishia makazi yake Singida
Singida Big Stars ikabadilishwa jina na kuwa Singida Fountain Gate na kuhamishia makazi yake jijini Mwanza yalipokuwa makazi ya wamiliki wapya walioinunua timu hiyo na kuibadili jina kuiita Fountain Gate
Imeitwa Pacha Derby kwa sababu wamiliki wa timu hizi walikuwa pamoja kabla ya sintofahamu iliyojitokeza baada ya Singida Big Stas kuuzwa



