Kifo cha shabiki chazuia shangwe la ushindi Bayern

Joel JJ By Joel JJ β€’ 8th November 2024


Kifo cha shabiki chazuia shangwe la ushindi Bayern

Kocha wa Bayern Munich, Vincent Kompany amesema kifo cha shabiki wao mmoja aliyekuwepo uwanjani juzi kutazama mchezo wao wa Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya Benfica kilisababisha wasishangilie baada ya mechi kumalizika kama ilivyo kawaida yao

Shabiki huyo alizidiwa jukwaani katika uwanja huo wa Allianz Arena na watu wa huduma ya kwanza walimpatia matibabu kwa dakika kadhaa kabla ya kumbeba kwenye machela kwa ajili ya kumuwahisha hospitali lakini akafariki dunia wakiwa njiani

Eneo ambalo shabiki huyo alidondoka na matibabu yakawa yanaendelea kulikuwa kimya baada ya mashabiki kunyamaza kwa muda mwingi wakati matibabu yanaendelea

Akizungumza baada ya mchezo huo ambao ulimalizika kwa kushinda 1-0, Kompany alisema;

"Ni vigumu kuzungumzia masuala ya soka kwa sasa, baada ya mchezo hatukusheherekea kama ilivyo kawaida yetu, bila shaka wachezaji nao walijua hilo, kuna dharura imetokea. Siku zote tunatumai mashabiki wetu na wote watarejea nyumbani wakiwa salama. Kwa bahati mbaya, haikuwa hivyo."

Kwa upande wake mshambuliaji wa timu hiyo, Thomas Muller alisema;

"Tuligundua hilo, tuliona hali ya uwanja na ushangiliaji ulikuwa tofauti, kundi lililokuwa likiruka ruka kabla ya mchezo baada ya kutokea kwa tukio hilo halikufanya hivyo. Nilifurahi kuona wameacha kushangilia kutokana na suala hilo, hiyo ni ishara nzuri ya mshikamano, mashabiki hawaweki timu mbele na ubinadamu pia wanazingatia"

Taarifa rasmi kutoka kwa timu hiyo ilisema;

"Katika mechi ya Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya Benfica, ushindi wetu wa 1-0 uligubikwa na tukio la kusikitisha baada ya kutokea kwa dharura ya kiafya kwa shabiki yetu, hiyo ilisababisha kundi la mashabiki la Sudkurve lisitishe ushangiliaji ili kuruhusu matibabu yaendelee na baada ya mechi kumalizika tulipata taarifa shabiki huyo alifariki dunia akiwa njiani kupelekwa hospitali"

Mwanaspoti


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.