Baada ya kuichapa Al Hilal bao 1-0 ugenini huko Mauritania na kurejesha matumaini ya kufuzu robo fainali ya ligi ya mabingwa barani Afrika (CAF CL), Kocha Mkuu wa Yanga Sead Ramovic amesitisha sherehe na kuwataka wachezaji wasahau ushindi dhidi ya Al Hilal kwani wanakabiliwa na mechi muhimu mwishoni mwa wiki dhidi ya MC Alger
Jumamosi, Januari 18 Yanga inahitaji kushinda mchezo dhidi ya MC Alger ili kufuzu robo fainali ya CAF CL
Ramovic amesema jambo muhimu kwao ni kuelekeza nguvu katika mchezo ambao anaamini utakuwa mgumu lakini wanapaswa kutumia vyema uwanja wa nyumbani kufuzu robo fainali
"Mechi dhidi ya Al Hilal imekwisha, nimewaambia wachezaji baada ya kutoka ndani ya uwanja kila mmoja asitishe furaha yake, tunatakiwa kujiona kama hatujafanya kitu na tukitakiwa kwenda kufanya kitu kikubwa zaidi kwenye mchezo ujao wa nyumbani"
"Tunatakiwa kushinda mechi ya mwisho kwa nguvu licha ya kwamba haitakuwa rahisi, MC Alger nao wanapitia mabadiliko kwenye timu yao tofauti na walivyoanza mechi za makundi, tunachotakiwa ni kuongeza umakini kwenye mechi hii ya mwisho"
"Tutakuwa nyumbani na wao walishinda dhidi yetu wakiwa kwao, nasi tunapaswa kushinda nyumbani"
"Tumekuwa na mabadiliko mazuri ndani ya timu yetu tofauti na mechi mbili za kwanza tulizocheza na tumeanza kuimarika kwa nguvu, nawapongeza sana wachezaji wangu, lakini wanatakiwa kutambua tunakwenda kucheza mechi ngumu itakayobeba heshima yetu," alisema Ramovic
Yanga inatarajiwa kutua leo wakitokea Addis Ababa, Ethiopia ambapo timu ilitua jana kutoka Mauritania msafara ukipata muda wa kupumzika kabla ya kuunganisha ndege ya kurejea nyumbani mchana wa leo



