Mwenyekiti wa klabu ya Simba Murtaza Mangungu amewataka mashabiki wa timu hiyo kukaa tayari kwa mchezo wa marudiano robo fainali ya kombe la Shirikisho(CAF CC) dhidi ya Al Masry ambao utapigwa Jumatano ijayo April 09 katika uwanja wa Benjamin Mkapa
Akizungumza baada ya mchezo wa mkondo wa kwanza uliopigwa Misri na Simba kukubali kipigo cha mabao 2-0, Mangungu alisema hayakuwa matokeo waliyotarajia lakini ari na morali iliyoonyeshwa na wachezaji katika mchezo huo, inawapa imani ya kushinda mechi ya marudiano na kufuzu nusu fainali
"Ukiangalia mchezo sisi tulitawala kwa kiasi kikubwa, ni bahati mbaya tumekosa magoli mengi ya wazi, tumetengeneza nafasi nyingi lakini hatukuwa na bahati ya kupata magoli"
"Naamini mwalimu na benchi la ufundi watakuwa na nafasi ya kufanyia kazi mapungufu yaliyojitokeza leo"
"Hii timu tuna uwezo wa kuifunga nyumbani, hata hapa tulikuwa na uwezo wa kuifunga lakini kwa bahati mbaya tu maamuzi nayo vilvile hayakuwa sahihi upande wetu"
"Kwenye michezo hii ya kiafrika tunakubaliana na hilo lakini sasa tunawasubiri waje nyumbani tuone na sisi tutautumiaje uwanja wetu wa nyumbani"
"Jambo kubwa kwa mashabiki, wanachama na wote wanaoitakia mema Simba kuweka nguvu ya pamoja na kufanya maandalizi ya nguvu kukabiliana nao. Hii ni timu ambayo tunao uwezo wa kuitoa na kusonga mbele hatua ya nusu fainali," alisema Mangungu



