Klabu ya Simba SC imewasili salama visiwani Zanzibar ikiwa na azma ya kutwaa taji lao la kwanza la Kombe la Shirikisho barani Afrika, watakapokipiga dhidi ya RS Berkane ya Morocco katika mchezo wa mkondo wa pili wa fainali utakaofanyika Jumapili, Mei 25, kwenye dimba la New Amaan Complex.
Kikosi kizima kilichosajiliwa msimu huu kilikuwa sehemu ya msafara uliotoka Dar es Salaam mapema leo, ikiwa ni ishara ya maandalizi makini kuelekea mchezo huu wa kihistoria.
Mchezo huo wa fainali utaanza majira ya saa 10 jioni, na mara baada yake, kutafanyika hafla rasmi ya kuhitimisha msimu wa michuano ya CAF Confederation Cup (CAF CC), ikiwa ni pamoja na utoaji wa medali na zawadi kwa washindi.
Wachezaji wa Simba tayari wana uhakika wa kuondoka na medali β aidha za dhahabu endapo watashinda, au fedha iwapo matokeo yatakuwa kinyume. Hata hivyo, msimamo wa kikosi cha Wekundu wa Msimbazi uko wazi: wanataka ushindi pekee.
Ni kumbukumbu inayochoma: mwaka 1993, Simba walipoteza fainali ya Kombe la CAF kwenye Uwanja wa Uhuru, wakishuhudia wageni wakitoka na kombe mikononi mwao. Safari hii, mbele ya mashabiki wao wenyewe, Mnyama hataki kurudia makosa ya zamani.
Kwa sasa, macho yote yanaelekezwa New Amaan Complex β ambapo historia mpya inaweza kuandikwa. Simba wanapigania si tu ushindi wa mechi, bali pia heshima ya Tanzania katika anga la soka la Afrika
Wakati Simba ikiwasili Zanzibar leo, wapinzani wao RS Berkane wnatarajiwa kuwasili visiwani humo siku ya Alhamis



