Fadlu ataka wapya sita Simba

Joel JJ By Joel JJ • 8th July 2025


Fadlu ataka wapya sita Simba

Hivi karibuni, Bodi ya Wakurugenzi ya Simba SC ilikamilisha kikao chake jijini Dar es Salaam, ambapo mojawapo ya mambo makuu yaliyajadiliwa ni ripoti ya benchi la ufundi iliyowasilishwa na kocha mkuu Fadlu Davids.

Ripoti hiyo inalenga kutoa mwelekeo wa maboresho muhimu ya kikosi ili kuhakikisha Simba inarejea msimu ujao ikiwa na nguvu kubwa ya kuwania mataji mbalimbali.

Katika ripoti hiyo, kocha Fadlu Davids ameeleza wazi kinachohitajika kufanyika kwenye usajili ili kuondoa mapungufu yaliyoathiri utendaji wa timu msimu uliomalizika, ambapo amependekeza kuongeza wachezaji sita wa kigeni ili kuboresha nafasi muhimu ndani ya kikosi.

Miongoni mwa mapendekezo makuu yaliyotolewa na kocha ni:

  • Kuongeza nguvu katika nafasi ya Jean Charles Ahoua na kuleta mchezaji mwingine anayeweza kuhimili jukumu la namba 10, ambaye atakuwa na uwezo wa kufunga magoli na kutoa pasi za mwisho kwa wenzake.

  • Kuongeza beki wa kati mwenye uwezo mkubwa wa kukaba kwa nguvu na akili, jambo muhimu kwa kuimarisha safu ya ulinzi.

  • Kuimarisha nafasi kiungo mkabaji mwenye uwezo wa juu zaidi kuliko Yusuph Kagoma ili kuboresha udhibiti wa mchezo kati ya viungo.

  • Kuleta winga mwenye uwezo mkubwa kuliko Joshua Mutale ili kuongeza kasi na ushindani upande wa pembeni.

  • Kuongeza mashambuliaji mmoja au wawili wenye uwezo mkubwa wa kupachika mipira ndani ya wavu, wakionekana kuwa na kiwango bora zaidi kuliko Leonel Ateba na Steven Mukwala.

Aidha, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi, Bilionea Mohammed Dewji ‘Mo’, amekuwa mstari wa mbele kuanzisha bodi ya ushauri kuhusu masuala ya usajili ambayo inahusisha viongozi wa zamani wa Simba SC pamoja na wachezaji waliowahi kuitumikia klabu kwa mafanikio makubwa.

Lengo ni kuhakikisha kuna wigo mpana wa kuwafanyia tathmini wachezaji wanaopendekezwa kabla ya kusaini mikataba, na hivyo kufanya usajili wa maana na wenye manufaa kwa timu.

Viongozi wa zamani kama Geofrey Nyange ‘Kaburu’, Hassan Dalali, Ismail Aden Rage, na Evance Aveva, ambao walijulikana kwa uwezo wao wa kuleta usajili bora licha ya kukosekana kwa rasilimali nyingi, wamehusishwa tena katika mchakato huu wa usajili.

Mmoja wa wajumbe wa bodi alisema,

“Hawakushirikishwa kwenye usajili wa msimu uliopita, lakini huu unaokwenda kufanyika na wao wapo, walikuwemo kwenye kikao, wamemshauri mwenyekiti wetu nini cha kufanya ili kupata kikosi chenye ubora na tishio.”


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.