Wakati akizungumza na wanahabari jana, Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Yanga Ali Kamwe alitoa 'code' ya kocha ambaye Yanga wamemuajiri kukiongoza kikosi cha mabingwa hao wa kihistoria katika msimu ujao
Kamwe alidokeza kuwa kocha huyo ni kijana na mwenye kiu ya mafanikio. Ni kocha ambaye anaendana na mahitaji ya Yanga yenye malengo ya kulisaka taji la Afrika
Kamwe alisema kocha huyo atatambulishwa mwishoni mwa mwezi huu kabla ya timu kuelekea kwenye maandalizi ya msimu mpya
Baada ya kauli ya Kamwe, tetesi zinamuhusisha Romain Folz mwenye umri wa miaka 35) mzaliwa wa Bordeaux huko Ufaransa
Licha ya umri wake mdogo, Romain ni kocha mwenye uzoefu mkubwa katika michuano ya Kimataifa akifanya kazi katika klabu mbalimbali kama kocha mkuu, kocha msaidizi au Mkurugenzi wa ufundi
Mwaka 2024 Folz alihudumu katika klabu ya Mamelodi Sundowns kama Kocha Msaidizi kabla ya kutimkia Algeria kuwa Mkurugenzi wa Michezo klabu ya Olympique Akbou
Folz pia amewahi kuzitumikia ya Guinea Horoya AC (Kocha Mkuu), Amazulu ya Afrika Kusini (Kocha Mkuu), Township Rollers ya Botswana (Kocha Mkuu), Pyramids ya Misri (Kocha Msaidizi) na timu ya Taifa ya Uganda (Kocha Msaidizi)
Folz ana leseni ya juu ya ukocha inayotolewa na UEFA (UEFA Pro Licence) na pia ana Pro Licence ya CONMEBOL
Ukiangalia umri wake na CV yake iliyoshiba, Folz ni kocha aliyewekeza katika kufundisha mpira wa miguu akihitimu mafunzo yake ya ukocha katika umri mdogo
Ni kocha mwingine kijana ambaye anaweza kupata nafasi ya kuinoa Yanga baada ya Cedric Kaze na Sead Ramovic ambao wote wakati wanatua Yanga hakuna aliyewafahamu
Kaze kwa sasa yuko na Nasreddine Nabi katika timu ya Kaizer Chiefs wakati muda mfupi wa kuitumikia Yanga ulitosha kumpa ulaji Ramovic aliyetimkia CR Belouizdad



