Klabu ya Simba SC huenda ikafanya maamuzi magumu kuhusu hatma ya mshambuliaji wao raia wa Cameroon, Lionel Ateba, kufuatia usajili mpya wa mshambuliaji wa kimataifa kutoka Ghana, Jonathan Sowah, aliyesajiliwa kutoka klabu ya Singida Black Stars.
Usajili wa Sowah, ambaye alifunga mabao 13 katika mechi 14 pekee msimu uliopita akiwa na Singida BS, unaifanya Simba kuwa na washambuliaji watatu wa kigeni: Jonathan Sowah, Steven Mukwala na Lionel Ateba.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka ndani ya klabu, Maghreb Fez ya Morocco tayari imetuma ofa rasmi kwa ajili ya kumsajili Ateba, na Simba huenda ikaisikiliza kwa ofa hiyo kama sehemu ya kupanga upya safu yake ya ushambuliaji.
Inaelezwa kuwa Kocha Mkuu wa Simba, Fadlu Davids, ameshathibitisha kumuhitaji Steven Mukwala kama sehemu muhimu ya mipango yake kwa msimu ujao. Mukwala, ambaye pia alifunga mabao 13 msimu uliopita, alimaliza msimu akiwa na kiwango bora Simba ikipuuzia ofa zote zilizowasilishwa kwa ajili yake.
Kwa upande mwingine, Lionel Ateba, licha ya kuwa na msimu mzuri akipachika mabao 13, anaonekana kuwa kwenye nafasi ya kupisha ujio wa Sowah.
Ushindani mkali unaotarajiwa kwenye eneo la ushambuliaji unaweza kumlazimu Mcamerooni huyo kutafuta nafasi ya kucheza zaidi nje ya Msimbazi.



