Yanga imeendelea kujichimbia kileleni mwa msimamo wa ligi kuu ya Tanzania Bara baada ya kuichapa Singida BS mabao 3-0 katika mchezo uliopigwa uwanja wa Airtel, Mtipa Singida.
Alikuwa ni Prince Dube aliyeibuka shujaa katika mchezo huo akifunga bao moja na kuhusika kwenye mabao mengine mawili.
Dube alifunga bao la uongozi dakika ya 41 akimalizia krosi ya Maxi Nzengeli. Dakika ya 45 Dube alifanyiwa madhambi ndani ya eneo la hatari na Chukwu mwamuzi akiamuru mkwaju wa penati uliowekwa kimiani na Allan Okello.
Kipindi cha pili Yanga iliendelea kutawala mchezo na kufanikiwa kuongeza bao la tatu kupitia kwa Mudathir Yahya akimalizia mpira uliotemwa na Metacha Mnata baada ya shuti la Dube.
Wananchi wamefikisha alama 32 baada ya mechi 12, wakizidi kusimika juu ya msimamo wa ligi.
Katika mchezo mwingine uliopigwa mkoani Mbeya, Azam Fc imelazimishwa suluhu ya bila kufungana dhidi ya Tanzania Prisons.
Huo ulikuwa mchezo wa pili mfululizo Azam Fc wanakosa ushindi ugenini baada ya kupata sare mchezo uliopita dhidi ya Pamba Jiji.
Licha ya kuwa nyuma ya mpira kwa muda mrefu, kocha mpya wa Prisons Shadrack Nsajigwa alifanikiwa kupata alama moja muhimu nyumbani.



