Mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya NBC, Yanga SC, wamerejea kileleni mwa msimamo wa ligi baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Fountain Gate katika mchezo uliopigwa kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid mjini Arusha.
Ushindi huo umeendelea kuonyesha ubora wa kikosi hicho katika mbio za kutetea ubingwa wao wa ligi, huku ukiwarejesha juu ya msimamo baada ya kuwa nyuma ya watani wao Simba kwa takribani saa 24 pekee.
Baada ya kipindi cha kwanza kumalizika kwa sare ya bila kufungana, Yanga walirejea uwanjani kwa kasi zaidi katika kipindi cha pili na kufanikiwa kupata mabao mawili yaliyowahakikishia pointi tatu muhimu.
Kiungo Pacรดme Zouzoua aliifungia Yanga bao la kwanza katika dakika ya 53 kabla ya mshambuliaji Depรบ kuongeza la pili dakika mbili baadaye, na kuzima kabisa matumaini ya Fountain Gate kurejea mchezoni.
Katika mchezo huo, Yanga walionyesha nidhamu kubwa ya kiuchezaji pamoja na umiliki mzuri wa mpira, hali iliyowapa nafasi ya kutawala sehemu kubwa ya mchezo dhidi ya wapinzani wao waliokuwa wakicheza mbele ya mashabiki wao.
Matokeo hayo yameifanya Yanga kufikisha pointi 66 na kurejea kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu ya NBC. Sasa kikosi hicho kinahitaji ushindi katika angalau mechi mbili pamoja na sare moja katika michezo iliyobaki ili kujihakikishia ubingwa wa tano mfululizo.
Pamba Jiji yashinda kwa kishindo, JKT yapigwa Isamuhyo
Katika mechi nyingine zilizochezwa leo, Pamba Jiji imeonyesha ubora wake kwa kuichapa Mtibwa Sugar mabao 4-0. Mshambuliaji Mathew Tegisi alikuwa nyota wa mchezo huo baada ya kufunga hat-trick ya pili katika Ligi Kuu msimu huu.
Hat-trick hiyo inakuja siku moja tu baada ya Mossi Ndumumwe wa Singida Black Stars kufunga hat-trick ya kwanza msimu huu.
Kwa upande mwingine, JKT Tanzania ilikumbana na matokeo yasiyotarajiwa baada ya kuchapwa bao 1-0 na Tanzania Prisons katika mchezo uliopigwa Uwanja wa Isamuhyo. Bao pekee la mchezo huo lilifungwa na George Mpole kupitia mkwaju wa penalti katika dakika ya 45, na kuipa Tanzania Prisons ushindi muhimu katika harakati zao za ligi.



