Timu ya taifa ya Ivory Coast imepoteza kwa maumivu makali mabao 2-1 dhidi ya Germany katika mechi ya Kundi E ya Kombe la Dunia 2026 iliyochezwa Toronto, Canada.
Ivory Coast ilianza vizuri na kufungua ukurasa wa mabao dakika ya 30 kupitia nahodha wake, Franck Kessié, baada ya shambulizi la haraka lililoongozwa na kijana mwenye kasi Yan Diomande. Bao hilo liliwapa matumaini makubwa "Tembo" kuelekea mapumziko wakiongoza 1-0.
Hata hivyo, Ujerumani ilirejea kwa nguvu kipindi cha pili baada ya kocha Julian Nagelsmann kufanya mabadiliko muhimu. Mshambuliaji wa akiba Deniz Undav aliisawazishia Ujerumani dakika ya 68 kwa mpira wa krosi kutoka kwa Nadiem Amiri.
Wakati mechi ilionekana kumalizika kwa sare, Undav aliibuka shujaa tena katika dakika ya 90+4 akifunga bao la ushindi baada ya pasi kutoka kwa Felix Nmecha. Bao hilo la dakika za mwisho liliwavunja moyo wachezaji na mashabiki wa Ivory Coast ambao walikuwa karibu kupata matokeo muhimu dhidi ya moja ya vigogo wa soka duniani.
Ushindi huo umeifanya Ujerumani kufikisha pointi sita na kufuzu hatua ya mtoano ya Kombe la Dunia, huku Ivory Coast ikibaki na pointi tatu baada ya mechi mbili. Matumaini ya Ivory Coast ya kusonga mbele bado yapo, lakini italazimika kupata matokeo mazuri katika mchezo wake wa mwisho wa kundi dhidi ya Curaçao.
Mbali na kipigo hicho, Ivory Coast pia ilipata pigo jingine baada ya beki wake muhimu Wilfried Singo kuumia wakati wa mchezo, jambo ambalo linaweza kuathiri maandalizi ya mechi ijayo.



